Tuesday, June 11, 2013

BALOZI WA MAREKANI NCHINI TANZANIA ADAI KUWA UJIO WA RAIS OBAMA SI KWA AJILI YA RASILIMALI ZA MTANZANIA


Akiongea na waandishi wa habari jana, Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Alfonso Lenhard amesema ziara ya mwezi ujao ya Rais wa Taifa la Marekani, Barack Obama nchini Tanzania haina ajenda ya siri: "kuna maswali mengi naulizwa kwa  nini Rais Obama amechagua kuzuru Tanzania? Ni kweli  Rais wetu anakuja malengo ya ziara yake yatajikita katika mambo ambayo ni malengo ya Marekani kwa Afrika, ambayo ni uhusiano wa kiuchumi, kuimarisha demokrasia na kuwekeza katika kujenga kizazi kijacho cha uongozi."
Akijibu swali aliloulizwa na mwandishi wa habari kuhusu uhusiano wa ujio wa Rais Obama na rasilimali za Tanzania, Balozi Lenhardt alisema: "Ni kweli Obama atakuja Tanzania. Lakini niwahakikishie tu kuwa haji kupora rasilimali za Tanzania, kwani Marekani ina rasilimali nyingi zinazojitosheleza..." 


“Watanzania ni watu wapole na wakarimu ila mna tatizo moja la kuhofia kila jambo. Kila kitu mnachofanyiwa mnaona kuna baya linakuja. Sisi tuna nia njema ya kuwasaidia kuendelea.”

Akizitaja sababu nne zilizosababisha Rais Obama kuichagua Tanzania, Lenhardt alisema:

  1. Tanzania  ni nchi pekee kati ya nchi tano za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), ambayo Obama amechagua kufanya ziara yake ya kikazi kutokana na kuwa mfano wa utawala bora, demokrasia na ushirikishaji wa watu wake wakati wa kufanya uamuzi unaogusa maisha yao ya kila siku. Akasema Tanzania ni nchi ya mfano linapokuja suala la uongozi bora na ndiyo maana imekuwa na amani na utulivu kwa muda mrefu ikilinganishwa na nchi nyingi za Kusini mwa Jangwa la Sahara: “Nchi nyingi za Afrika zinazoizunguka Tanzania zimekuwa na matatizo ya vita vya wenyewe na hata ukosefu wa utawala bora,” alisema Balozi Lenhardt ingawa alidokeza kuwa katika siku za karibuni imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali kutokana na matukio ya uvunjifu wa amani.
  2. Jitihada za Serikali ya Marekani kutengeneza mazingira mazuri ya uwekezaji na kasi ya ukuaji wa uchumi: “Rais Obama anakuja kuunga mkono juhudi za Watanzania katika kutengeneza mazuri ya uwekezaji lakini bila kusahau kuwa kasi ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania imeivutia Serikali ya Marekani.”
  3. Kuisaidia Tanzania kuendeleza fursa mbalimbali za kujiletea maendeleo. Alisema uendelezaji huo wa fursa una lengo la kuisaidia Serikali ya Tanzania kukabiliana na tatizo la umaskini na kwamba Marekani ni moja ya nchi zinazoongoza kwa kutoa fedha nyingi za misaada na akisema kwa mfano, mwaka 2012 pekee ilitoa Dola 750 milioni. Aidha, alisema nchi yake imekuwa ikitoa misaada mingi kupitia Shirika la Millenium Challenge (MCC), ambayo imejikita zaidi katika kusaidia sekta za umeme, maji na miundombinu. Alisema Tanzania inaunga mkono jitihada za Serikali kujitosheleza kwa chakula na inafadhili Mkakati wa Kukuza Kilimo Kusini mwa Tanzania (SAGCOT): “Tunaunga mkono mpango wa SAGCOT kupitia Mfuko wa Rais wa Marekani unaoitwa `Feed the Future’ lengo likiwa kuifanya Tanzania kupiga hatua katika kilimo,” alisema balozi huyo.
  4. Kuhimiza haja ya Afrika kutayarisha viongozi wa kizazi kijacho. Ameanzisha programu ya kuandaa viongozi wa kizazi inayoitwa `Young African Leaders Initiative’ na Watanzania watatu, Modesta Lilian Mahiga, Masoud Salim Mohamed na Malula Hassan Nkanyemka walishiriki katika mpango huo na kukutana na kiongozi huyo mwaka 2010: “Rais Obama anataka kusaidia kuandaa viongozi wa kizazi kijacho wa Afrika kusimamia vizuri rasilimali za nchi,” alisema.

"Tunaweza tusitoe taarifa za kina juu ya ziara hii, kwani mambo yote yanaratibiwa na Ikulu ya Marekani, lakini niseme kwamba sisi tunahitaji kuwa na marafiki na Tanzania ni rafiki yetu na sio suala la kuchukua rasilimali zenu..."

 
 "Hatuna ajenda ya siri juu ya ziara hiyo. Ila kampuni za Marekani zimekubali kuja nchini kwa ajili ya kuangalia fursa za kuwekeza na lazima zitafuata taratibu zote..." alisema Lenhardt na kuongeza kuwa akiwa nchini, Obama atakutana na viongozi wa Serikali, wafanyabiashara na asasi zisizo kuwa za kiserikali ambazo ni muhimu katika ustawi wa nchi hasa katika maeneo tajwa hapo juu, alisisitiza Balozi huyo.  

USHINDANI NA CHINA

Rais wa China, Xi Jinping aliitembelea Tanzania Machi mwaka huu na ujio wa Obama umetafsiriwa na baadhi ya watu kuwa ni ushindani wa mataifa hayo mawili katika kusaka na kunufaika na rasilimali za Afrika.


Akizungumzia ushindani na China kuhusiana na fursa za kuwekeza na kuvuna rasilimali za Afrika, Balozi Leinhardt alisema imani yao ni kuwa China inadumisha urafiki na Tanzania kwa nia ya kuisaidia kuendelea... “Sisi hatuna shida na China, kwani tunaamini wako kwa ajili ya kusaidia. Ilimradi tu wawe na dhamira safi katika kuwasaidia.”


Nchi nyingine atakazozuru Rais Obama ni Senegal na Afrika Kusini. Ataanza ziara ya kutembelea nchi hizo tatu Juni 26 — Julai 2, 2013.


Katika safari hiyo, Obama atafuatana na mkewe, Michele na wanawe,  Sasha na Malia. Atakuwa Rais wa tatu wa Marekani kuitembelea Tanzania baada ya Bill Clinton mwaka 2000 na George Bush mwaka 2008.

No comments:

Post a Comment