Thursday, May 23, 2013

ASKARI ALIYENASWA NA MAGUNIA 18 YA BANGI HUKO HIMO AWATOROKA POLISI



ASKARI Polisi Koplo Edward, anayedaiwa kusafirisha dawa za kulevya (bangi) gunia 18 huko Himo, Kilimanjaro tarehe 18, Mei 2013, ametoroka chini ya ulinzi wa askari polisi saba na kutokomea kusikojulikana.

Mtuhumiwa huyo alikuwa dereva wa gari aina ya Toyota Landcruiser namba PT. 2025 la Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) Mkoa wa Arusha. 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema askari huyo akiwa chini ya ulinzi wa askari polisi saba, walikwenda nyumbani kwake kwa ajili ya ukaguzi, na walipofika nyumbani kwa  mtuhumiwa, walimwamini na kumwacha kuingia ndani peke yake nao waliingia ndani ili kuendelea na upekuzi, na ndipo mtuhumiwa alipofungua mlango wa nyuma ya nyumba yake na kukimbia bila ya wao kufanikiwa kumkamata
 

Alisema polisi imemkamata Inspekta wa Polisi Izaack Manoni aliyekuwa anasimamia upekuzi huo: “Inspekta Manoni yupo chini ya ulinzi na hatua za kinidhamu dhidi yake zitachukuliwa,” alisema ACP Sabas na kuongeza:  
“Mtuhumiwa Edward, anayetafutwa kwa sasa alishafukuzwa kazi, akipatikana atafikishwa mahakama ya kiraia kusomewa mashitaka ya kufanya biashara ya dawa za kulevya,” alisema.

Alisema tayari mtuhumiwa mwenzake ambaye ni askari polisi mwenye namba G. 2434 PC George, amesomewa mashitaka yake jana.

Mbali na mtuhumiwa huyo, watuhumiwa wengine waliokamatwa na magunia 30 ya bangi wilayani Arumeru nao wamepandishwa kizimbani kusomewa mashitaka yao.

No comments:

Post a Comment